Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) linautaarifu umma kuwa Udahili wa wanafunzi kwa mwaka wa masomo 2025/2026 kwa ngazi ya Astashahada na Stashahada katika kozi zote zinazosimamiwa na NACTVET umefunguliwa rasmi leo tarehe 28 Mei, 2025.
Maombi ya udahili kwa kozi zisizo za Afya na Sayansi Shirikishi, na kozi za Afya na Sayansi Shirikishi zitolewazo katika vyuo vilivyoko Zanzibar yatumwe moja kwa moja kwenye vyuo husika kuanzia tarehe 28 Mei hadi tarehe 11 Julai, 2025.
Aidha, maombi ya kozi za Afya na Sayansi Shirikishi – Tanzania Bara, yatafanyika kupitia Mfumo wa Udahili wa Pamoja (Central Admission System-CAS) unaopatikana katika tovuti ya Baraza (www.nactvet.go.tz) kuanzia tarehe 28 Mei hadi tarehe 11 Julai, 2025.
Baraza pia linautaarifu umma kuwa kozi zinazoombwa na vyuo vinavyotoa kozi hizo vimeorodheshwa kwenye Kitabu cha Mwongozo wa Udahili kwa Mwaka wa Masomo 2025/2026 (Admission Guidebook for Academic Year 2025/2026). Mwongozo huo unapatikana katika tovuti ya Baraza (www.nactvet.go.tz).
Baraza linasisitiza kila mwombaji kuhusika mwenyewe katika zoezi zima la kuomba kudahiliwa, kuandika taarifa zake kwa usahihi na umakini, na kutunza kumbukumbu atakazopatiwa na Baraza kupitia namba yake ya simu, bila kumpatia mtu mwingine yeyote ili kuepuka usumbufu katika zoezi zima la maombi ya kujiunga na kozi/vyuo mbalimbali.
Mambo ya Kuzingatia kwa Wanaoomba Kupitia Mfumo wa Udhaili wa Pamoja (Central Admission System – CAS):
- Muombaji anaweza kuomba chuo zaidi ya kimoja. Kuchaguliwa katika chuo alichoomba kutategemea ushindani utakaokuwepo katika chuo hicho.
- Muombaji akishachaguliwa, atapokea ujumbe kutoka NACTVET kupitia namba ya simu yake aliyoweka kwenye mfumo wakati wa kufanya maombi. Ujumbe huo utamjulisha kuwa amechaguliwa kujiunga na chuo fulani (jina la chuo), na utakuwa na msimbo (code) ambao atatakiwa kuutunza na kuuwasilisha kwa chuo alichochaguliwa siku atakapokwenda katika chuo hicho kwa ajili ya kuanza masomo.
- Baada ya kuwasilisha msimbo huo chuoni, atasajiliwa na chuo, kisha atapokea ujumbe kutoka NACTVET ukimueleza kuwa amesajiliwa.
- Baada ya kusajiliwa, mwanafunzi aingie katika tovuti ya NACTVET (www.nactvet.go.tz), kisha ajiridhishe kuwa amesajiliwa kwa kuhakiki taarifa zake kwa kubonyeza “link” inayosomeka “student’s information verification”.
Mambo ya Kuzingatia kwa Wanaoomba Moja kwa Moja Vyuoni:
- Muombaji anaweza kuomba chuo zaidi ya kimoja. Kuchaguliwa katika chuo alichoomba kutategemea ushindani utakaokuwepo katika chuo hicho.
- Muombaji akishachaguliwa na chuo, chuo husika kitawasilisha taarifa za muombaji NACTVET kwa ajili ya uhakiki. Muombaji atapokea ujumbe ukimtaarifu kuwa taarifa zake zimewasilishwa NACTVET na chuo kwa ajili ya kuhakikwa
- Baada ya taarifa zake kuhakikiwa, atapokea ujumbe kutoka NACTVET ukimjulisha kuwa amehakikwa, na utakuwa na msimbo (code) ambao atatakiwa kuutumia kuangalia taarifa zake za uhakiki. Pia atatakiwa kuutunza msimbo huo na kuuwasilisha kwa chuo alichochaguliwa siku atakapokwenda katika chuo hicho kwa ajili ya kuanza masomo.
- Baada ya kuwasilisha msimbo huo chuoni, atasajiliwa na chuo, kisha atapokea ujumbe kutoka NACTVET ukimueleza kuwa amesajiliwa.
- Baada ya kusajiliwa, mwanafunzi anatakiwa aingie katika tovuti ya NACTVET (www.nactvet.go.tz), kisha ajiridhishe kuwa amesajiliwa kwa kuhakiki taarifa zake kwa kubonyeza “link” inayosomeka “student’s information verification”.