Dodoma – Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limetoa tangazo la nafasi za kujiunga na jeshi hilo kwa vijana wa Kitanzania wenye sifa za elimu kuanzia sekondari hadi chuo kikuu.
Tangazo hilo limetolewa leo Jumatano tarehe 30 Aprili, 2025 na Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano wa JWTZ, Kanali Gaudentius Ilonda, alipokuwa akizungumza na wanahabari makao makuu ya jeshi jijini Dodoma.
Kwa mujibu wa Kanali Ilonda, JWTZ linahitaji wataalamu mbalimbali wa afya ikiwemo madaktari bingwa wa upasuaji, upasuaji wa mifupa, magonjwa ya kibofu, wataalamu wa picha za kitabibu kama vile X-ray, MRI na CT scan, madaktari wa masikio, pua na koo, wa usingizi, magonjwa ya ndani, macho, saratani, tiba za dharura na damu; pamoja na madaktari wa magonjwa ya akili na wataalamu wa uchunguzi wa sampuli za mwili. Kadhalika, nafasi zimefunguliwa kwa wataalamu wa huduma za wanyama, wahandisi wa tiba na vifaa tiba, na wataalamu wa maabara ya meno pamoja na madaktari wa afya za abiria na wahudumu wa anga.
Aidha, JWTZ inawakaribisha mafundi wa aluminium welding, welding na metal fabrication kuwasilisha maombi yao.
Kanali Ilonda amebainisha kuwa waombaji wanatakiwa kuwa raia wa Tanzania wenye kitambulisho cha taifa, afya njema na akili timamu, ambao hawajawahi kutiwa hatiani kwa kosa lolote la jinai. Waombaji wote wanapaswa kuwa na vyeti halisi vya kuzaliwa, vya masomo na taaluma husika, na wawe hawajawahi kuhudumu kwenye Jeshi la Polisi, Magereza, au Kikosi cha Kuzuia Magendo.
Sharti lingine ni kwamba mwombaji awe amehitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) au kwa mujibu wa sher ia na awe na cheti cha uthibitisho. Kigezo cha umri kwa waliohitimu kidato cha nne na sita ni miaka isiyozidi 24; stashahada wasiwe na zaidi ya miaka 26; elimu ya juu wasiwe na zaidi ya miaka 27; na madaktari bingwa isiwe zaidi ya miaka 35.
Maombi yote yaandikwe kwa mkono na kuwasilishwa makao makuu ya JWTZ Dodoma kati ya Mei 1 hadi Mei 14, 2025. Waombaji watume maombi yao yakiwa na nakala ya kitambulisho cha Taifa au namba ya NIDA, nakala ya cheti cha kuzaliwa, vyeti vya shule na chuo, hati ya kumaliza JKT (kwa waliohitimu mafunzo hayo), pamoja na namba ya simu ya mkononi.